Mkuu wa mkoa wa Mtwara Kanali Ahmed Abbas Ahmed amefanya ziara ya siku moja katika wilaya ya Tandahimba kukagua maendeleo katika sekta ya elimu ili kujiridhisha na takwimu za uandikishaji wa wanafunzi wa kidato cha kwanza.
Katika ziara hiyo Kanali Abbas pia amekagua mradi wa vyumba vine vya madarasa uliogharimu kiasi cha Tsh. Milioni 80 katika shule ya sekondari ya Tandahimba ambapo ameonesha kuridhishwa na utekelezaji wa mradi huo.
“Ndugu zangu wana Tandahimba vyumba hivi vinne mnavyoviona mbele yenu ni sehemu ya mradi wa vyumba 134 ambavyo Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, aliutengea mkoa wetu kiasi cha Tsh bilioni 2.6 kutekeleza mradi wa kuboresha miundombinu katika shule zetu za sekondari kama njia ya kuwasaidia wanafunzi wa kidato cha kwanza” alisema Kanali Abbas.
Aidha Kanali Abbas amewataka viongozi wa wilaya pamoja na walimu kuendelea kusimamia ipasavyo sekta ya elimu wilayani humo kama njia ya kusaidia kupata matokeo mazuri ya wanafunzi.
“nichukue fursa hii kuwapongeza sana kwa matokeo mazuri ya kidato cha nne mliyoyapata, bila shaka hii ni ishara nzuri kwa wilaya yenu kuwa na kiu ya kufanya vizuri zaidi katika siku za usoni” aliongeza Kanali Abbas.
Halikadhalika Kanali Abbas ameitumia fursa hiyo kuwahimiza walimu kusimamia vema suala la utunzaji wa mazingira ya shule hiyo ili yafanane na ubora wa miundombinu yake.
Pia mkuu wa mkoa Kanali Ahmed Abbas Ahmed alikagua ujenzi wa zahanati uliotekelezwa kwa nguvu za wananchi katika kata ya Mnyawi, ambapo aliunga mkono jitihada hizo kwa kukabidhi vifaa vya ujenzi ikiwemo mabati 200 na mifuko 20 ya sementi, vifaa ambavyo ni michango ya viongozi mbalimbali wa wilaya ya Tandahimba.
MWISHO.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Mtwara
Anuani ya Posta: 544, MTWARA
Simu: +255 23 2333014
Mobile: +255 23 2333014
Barua Pepe: ras@mtwara.go.tz
Haki Miliki © 2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Mtwara. Haki zote zimehifadhiwa.