Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Isdor Mpango, leo Julai 26, 2021 ametembelea Bandari ya Mtwara na kujionea ujenzi wa gati mpya uliofanywa bandari hapo kwa kugharimu shiling bilioni 157. Akiwa bandarini hapo Mkamu wa Rais amesema Serikali ya awamu ya Sita imejipanga kuhakikisha kuwa Bandari ya Mtwara inatumika ipasavyo ili kuinua uchumi wa mkoa wa Mtwara na Taifa kwa ujumla. Ameuagiza uongozi wa Mamlaka ya Bandari kuendelea kutafuta masoko katika nchi jirani kama vile Msumbiji, Malawi na Comoro ili kuongeza wigo wa matumizi ya bandari ya Mtwara na kuliongezea taifa mapato.
Aidha Makamu wa Rais ameitaka Wizara ya Kilimo, kuhakikisha mazao yote yanayolimwa Mikoa ya Kusini ya Ruvuma, Mtwara na Lindi kama vile mbaazi,ufuta na Korosho yasafirishwe kupitia Bandari ya Mtwara badala ya Bandari ya Dar es Salaam kuanzia msimu ujao. Pia ameitaka Wizara ya Kilimo na Wizara ya Ujenzi na uchukuzi kuhakikisha kwamba pembejeo za korosho zinapitia Bandari ya Mtwara na siyo bandari ya Dar es Salaam na utaratibu huu kuwa wa kudumu kuanzia sasa. Kwa upande wake Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Mhandisi Leonard Chamriho amesema tayari bandari hiyo ipo tayari kupokea meli zote zinazobeba shehena ya mizigo kwaajili ya mikoa ya kusini nan chi jirani na tayari wanafanya mazungumzo na kampuni mbalimbali ili kuzishawishi kutumia bandari hiyo.
Katika hatua nyingine Makamu wa Rais ametembelea na kuweka jiwe la msingi mradi wa chujio la maji Mangamba unaogharimu shilingi bilioni 2.3. Mradi huo unatarajiwa kutatua changamoto ya upatikanaji wa maji safi na salama mkoani Mtwara. Makamu wa Rais ameagiza mradi huo kukamilika mwezi Septemba kama ilivyopangwa hapo awali ili wananchi waanze kupata maji safi na salama. Aidha ameagiza wizara ya maji kutumia malighafi za ndani ya nchi katika ujenzi wa miradi mbalimbali hapa nchini.
Pia Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Isdor Mpango ameweka jiwe la msingi Hospitali ya Rufaa Kanda ya Kusini iliopo Manispaa ya Mikindani mkoani Mtwara, Leo Julai 26,2021, Mradi unaogharimu jumla ya Shilingi Bilioni 15.8. Hospitali ya Rufaa Kanda ya Kusini itahudumia mikoa ya Kusini ya Mtwara, Lindi na Ruvuma.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Mtwara
Anuani ya Posta: 544, MTWARA
Simu: +255 23 2333014
Mobile: +255 23 2333014
Barua Pepe: ras@mtwara.go.tz
Haki Miliki © 2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Mtwara. Haki zote zimehifadhiwa.