Wakazi wa mkoa wa Mtwara wakiongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Mtwara, Mhe. Abdallah Mwaipaya kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa leo tarehe 31 Mei 2025 wamepanda miti ya mikoko 6,000 pamoja na kufanya usafi wa mazingira katika pwani ya Miseti-Chuno ikiwa ni kampeni ya utunzaji wa mazingira kuelekea siku ya mazingira duniani.
Akizindua zoezi hilo la usafi wa mazingira na kupanda miti lililotanguliwa na mazoezi ya kukimbia (jogging) Mhe. Mwaipaya amewataka wananchi kutunza mazingira siku zote huku akitaka utaratibu kwa wananchi kufanya jogging na usafi wa mazingira kila Jumamosi ya mwisho wa mwezi urejeshwe.
“Tukiwa na mazingira ambayo si safi, nyasi kutuama katika mazingira tunakaribisha mazalia ya mbu anaesababisha ugonjwa hatari wa Malaria” Alieleza Mhe. Mwaipaya.
Aidha, DC Mwaipaya amemuagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara Mikindani kuwapa vifaa vya vya usafi kikundi cha usafi wa mazingira kiitwacho Miseti Women Group ili waweze kufanya kazi vema.
Kilele cha maadhimisho ya siku ya Mazingira duniani kitaifa yatafanyika tarehe 05 Juni 2025 jijini Dodoma ambapo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa mgeni rasmi.
Kimataifa maadhimisho haya yatafanyika nchini India katika mji wa New Delhi. Kaulimbiu inayoongoza maadhimisho haya ni “Beat Plastic Pollution”. Kaulimbiu hii inahimiza jamii kuepuka uchafuzi wa mazingira utokanao na plastiki.
Tanzania imepiga hatua katika kudhibiti taka za plastiki baada ya kupiga marufuku uzalishaji, uingizaji, usambazaji na matumizi ya mifuko ya plastiki kuanzia Juni, 2019, hatua iliyosaidia kupunguza uchafuzi wa mazingira.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Mtwara
Anuani ya Posta: 544, MTWARA
Simu: +255 23 2333014
Mobile: +255 23 2333014
Barua Pepe: ras@mtwara.go.tz
Haki Miliki © 2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Mtwara. Haki zote zimehifadhiwa.