Waziri wa Ujenzi, Mhe. Abdallah Ulega ameziagiza TANROAD na TARURA kuhakikisha wanawasimamia wakandarasi ili waweze kutoa ajira kwa wananchi wazawa pindi wanapotekeleza miradi ya ujenzi wa barabara na madaraja.
Waziri Ulega ametoa agizo hilo mapema leo tarehe 27 Mei 2025 alipotembelea na kukagua mradi wa ukarabati wa barabara ya Mtwara-Mingoyo (Mnazi mmoja) yenye urefu wa km 82 kwa thamani ya Shilingi Bilioni 152 na ile ya Mingoyo-Masasi yenye urefu wa Km 118 kwa thamani ya Bilioni 249.
“Afisa Rasilimali watu uhakikishe vijana wa hapa wanapata ajira, wakati wa kutoa ajira mshirikishe ofisi ya Mkuu wa Wilaya na serikali kwa ujumla, maafisa kazi waje hapa ili mwisho tuweze kujua mradi umeleta ajira ngapi kwa wananchi wetu.” Alisema Waziri Ulega
Akiongea na wafanyakazi wa mradi huo Mhe. Ulega alisema “Barabara hii si ya mchina, ni yetu watanzania, msifanye udokozi, fanyeni kazi kwa kujituma ili mradi unapoisha muwe mmepata maarifa ambayo yatakusaidia kuwa fundi mzuri.”
Waziri Ulega ameeleza kuwa tayari Serikali imeanza mchakato wa kuwarasimisha mafundi wasio rasmi ambao hawajapita kwenye vyuo vya mafunzo ya ufundi ila wana uzoefu wa ujenzi ili wapewe ajira hivyo kuzitaka mamlaka pamoja na wakandarasi kutoa vyeti kwa wafundi pindi mradi unapokamilika vitakavyowawezesha kutambuliwa.
Aidha, Waziri Ulega amemtaka mkandarasi huyo kufanya kazi kwa wakati na kwa ubora kwani tayari Serikali imeshamlipa malipo ya awali.
Kwa niaba ya wana Mtwara, Mkuu wa Mkoa, Mhe. Kanali Patrick Sawala amemshukuru Waziri Ulega pamoja na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuifungua Mtwara kwa miradi mbalimbali ya maendeleo.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Mtwara
Anuani ya Posta: 544, MTWARA
Simu: +255 23 2333014
Mobile: +255 23 2333014
Barua Pepe: ras@mtwara.go.tz
Haki Miliki © 2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Mtwara. Haki zote zimehifadhiwa.