Nchi nane za Afrika zimekutana mkoani Mtwara kwa mafunzo ya siku tano kuhusu mnyororo wa zao la korosho yanayojumuisha uzalishaji, ubanguaji, uongezaji thamani, sera, mabadiliko ya hali ya hewa, ushindaji wa korosho bara la Afrika na ulimwenguni kote.
Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Mhe. Kanali Patrick Sawala leo tarehe 23 Juni 2025 akifungua mafunzo hayo yanayosimamiwa na African Cashew Alliance amemshukuru na kumpongeza Waziri wa Kilimo, Mhe. Hussein Bashe kwa kusimamia vema sekta ya kilimo pamoja na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna anavyosaidia kilimo cha korosho kwa kutoa pembejeo bure, ajira kwa maafisa ugani na upatikanaji wa masoko ya uhakika.
Mkurugenzi wa Bodi ya Korosho Tanzania, Bw. Alfred Francis amesema Tanzania inashika nafasi ya tano kwa uzalishaji wa korosho duniani na nafasi ya pili kwa Afrika ikiongozwa na nchi ya Ivory Cost.
“Mafunzo haya yamekuja wakati muafaka kwetu Tanzania kwani tayari tumeanza jitihada za kuinua zao la korosho na mkulima kwa ujumla. Tunajenga kongani la viwanda vya kubangua korosho na maghala kule Maranje, tumeajiri maafisa ugani zaidi ya 500 kwahiyo mafunzo haya yatafanya tupige hatua kubwa zaidi kwenda kwenye mafanikio.” Alisema Bw. Alfred
Nae Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI) Dkt. Sophia Kashenge alisema “Kwetu korosho ni kila kitu, watu wanaongezeka lakini mabadiliko ya tabia ya nchi yanatuathiri, rutuba katika ardhi inapungua kwa kasi na hii ndo sababu inabidi tushirikiane sote kwa pamoja kuhakikisha mkulima anaongeza uzalishaji”
Katika hatua nyingine imeelezwa kuwa Tanzania itakuwa mwenyeji mkutano wa wa mwaka na maonesho ya 19 ya zao la korosho kwa mataifa ya Afrika, Carribean na Pasifiki utakaofanyika tarehe 18-22 Novemba 2025 ambapo kauli mbiu itakuwa “Wekeza kwenye korosho kwa maendeleo endelevu”.
Nchi zinazoshiriki mafunzo hayo ni pamoja na Tanzania, Kenya, Ghana, Sudan Kusini, Msumbiji, Uganda, Rwanda na Zambia.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Mtwara
Anuani ya Posta: 544, MTWARA
Simu: +255 23 2333014
Mobile: +255 23 2333014
Barua Pepe: ras@mtwara.go.tz
Haki Miliki © 2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Mtwara. Haki zote zimehifadhiwa.